MASOMO YA MISA


Septemba 11, 2024
Juma la 23, Mwaka B wa kanisa

SOMO: 1Kor 7:25–31

Kwa habari za wanawali sina amri ya Bwana, lakini natoa shauri langu, mimi niliyejaliwa kwa rehema za Bwana kuwa mwaminifu. Basi, naona hili kuwa jema, kwa ajili ya shida iliyopo, kwamba ni vema mtu akae kama alivyo.
Je! Umefungwa kwa mke? Usitake kufunguliwa. Umefunguliwa? Usitafute mke. Lakini, kama ukioa, huna hatia; wala mwanamwamli akiolewa, hana hatia; lakini watu kama hao watakuwa na dhiki katika mwili; name nataka kuwazuilia hayo. Lakini, ndugu, nasema hivi, muda ubakio si mwingi; basi tokea sasa wale walio na wake na wawe kama hawana; na wale waliao kama hawalii; na wale wafurahio kama hawafurahi; na wale wanunuao, kama hawana kitu. Na wale wautumiao ulimwengu huu, kama hawautumii sana; kwa maana mambo ya ulimwengu huu yanapita.

Neno la Bwana...Tumshukuru Mungu


WIMBO WA KATIKATI
Zab 45:10–11, 13–16

Sikia, binti, utazame, utege sikio lako,
Uwasahau watu wako na nyumba ya baba yako.
Naye mfalme atautamani uzuri wako,
Maana ndiye bwana wako, nawe umsujudie.
(K) Sikia, binti, utazame, utege sikio lako.

Binti mfalme yumo ndani ana fahari tupu,
Mavazi yake ni nyuzi za dhahabu.
Atapelekwa kwa mfalme
Wanawali wenzake wanaomfuata.
(K) Sikia, binti, utazame, utege sikio lako.

Watapelekwa kwa furaha na shangwe,
Na kuingia katika nyumba ya mfalme.
Badala ya baba zako watakuwapo watoto wako,
Utawafanya kuwa wakuu katika nchi zote.
(K) Sikia, binti, utazame, utege sikio lako.

SHANGILIO
Zab 119:105

Aleluya, aleluya,
Neno lako ni taa ya miguu yangu, na mwanga wa njia yangu.
Aleluya

INJILI
Lk 6:20–26

Yesu aliinua macho yake akawatazama wanafunzi wake, akasema, Heri ninny imlio maskini, kwa sababu ufalme wa Mungu ni wenu. Heri ninyi mlio na njaa sasa, kwa sababu mtashiba. Heri ninyi mliao sasa, kwa sababu mtacheka. Heri ninyi watu watakapowachukia na kuwatenga, na kuwashutumu, na kulitupa nje jina lenu kama neno ovu, kwa ajili ya Mwana wa Adamu.
Furahiwani siku ile na kuruka-ruka, kwa kuwa, tazama, thawabu yenu ni kubwa mbinguni; maana, baba zao waliwatenda manabii vivyo hivyo. Lakini, ole wenu ninyi mlio na mali, kwa kuwa faraja yenu mmekwisha kuipata. Ole wenu ninyi ambao mmeshiba sasa, kwa kuwa mtaona njaa. Ole wenu ninyi mnaocheka sasa, kwa kuwa mtaomboleza na kulia. Ole wenu ninyi watu wote watakapowasifu, kwa kuwa baba zao waliwatenda manabii wa uongo mambo kama hayo.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo.





Septemba 10, 2024
Juma la 23, Mwaka B wa kania
Mt. Apollinari Franco

SOMO: 1Kor 6:1–11

Je! Mtu wa kwenu akiwa ana dawa juu ya mwenzake athubutu kushitaki mbele ya wasio haki wala si mbele ya watakatifu? Au hamjui ya kwamba watakatifu watauhukumu ulimwengu? Na ikiwa ulimwengu utahukumiwa na ninyi, je! Hamstahili kukata hukumu zilizo ndogo? Hamjui ya kuwa tutawahukumu malaika, basi si zaidi sana mambo ya maisha haya? Basi, mkiwa na mahali panapohukumiwa mambo ya maisha haya, mwawaweka kuwa waamuzi hao waliohesabiwa kuwa si kitu katika kanisa? Nasema hayo nipate kuwatahayarisha. Je! Ndivyo, kwamba kwenu hakuna hata mtu mmoja mwenye hekima, awezaye kukata maneno ya ndugu zake? Bali mwashitakiana, ndugu kwa ndugu, tena mbele yao wasioamini. Basi imekuwa upungufu kwenu kabisa kwamba mnashitakiana ninyi kwa ninyi. Maana si afadhali kudhulumiwa? Maana si afadhali kunyang’anywa mali zenu? Bali kinyume cha hayo ninyi wenyewe mwadhulumu watu na kunyang’anya mali zao; naam, hata za ndugu zenu. Au hamjui ya kuwa wadhalimu hawataurithi ufalme wa Mungu? Msidanganyike; waasherati hawataurithi ufalme wa Mungu, wala waabudu sanamu, wala wazinzi, wala wafiraji, wala walawiti, wala wevi, wala watamanio, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang’anyi. Na baadhi yenu mlikuwa watu wa namna hii; lakini mlioshwa, lakini mlitakaswa, lakini mlihesabiwa haki katika jina la Bwana Yesu Kristo, na katika Roho wa Mungu wetu.

Neno la Bwana...Tumshukuru Mungu


WIMBO WA KATIKATI
Zab 149:1b-6a, 9b

Aleluya.
Mwimbieni Bwana wimbo mpya,
Sifa zake katika kusanyika la watauwa.
Israeli na amfurahie Yeye aliyemfanya,
Wana wa Sayuni na wamshangilie mfalme wako.
(K) Bwana awaridhia watu wake.

Na walisifu jina lake kwa kucheza,
Kwa matari na kinubi wamwimbie.
Kwa kuwa Bwana awaridhia watu wake,
Huwapamba wenye upole kwa wokovu. (K)

Watauwa na waushangilie utukufu,
Waimbe kwa sauti kuu vitandani mwao.
Sifa kuu za Mungu na ziwe vinywani mwao,
Hiyo ndiyo heshima ya watauwa wake wote.
Aleluya. (K)

SHANGILIO
Zab 111:7,8

Aleluya, aleluya,
Maagizo yako yote, Ee Bwana, ni amini, yamethibitika milele na milele.
Aleluya

INJILI
Lk 6:12-19

Yesu aliondoka akaenda mlimani ili kuomba, akakesha usiku kucha katika kumwomba Mungu. Hata kulipokuwa mchana aliwaita wanafunzi wake; akachagua kumi na wawili miongoni mwao, ambao aliwaita Mitume; Simoni, aliyemwita jina la pili Petro, na Andrea nduguye, na Yakobo na Yohane, na Filipo na Bartolomayo, na Mathayo na Tomaso, na Yakobo wa Alfayo, na Simoni aitwaye Zelote, na Yuda wa Yakobo, na Yuda Iskariote, ndiye aliyekuwa msaliti.
Akashuka pamoja nao, akasimama mahali tambarare, pamoja na wanafunzi wake wengi, na makutano makubwa ya watu waliotoka Uyahudi wote na Yerusalemu, na pwani ya Tiro na Sidoni; waliokuja kumsikiliza na kuponywa magonjwa yao; na wale waliosumbuliwa na pepo wachafu; waliponywa. Na makutano yote walikuwa wakitaka kumgusa, kwa sababu uweza ulikuwa ukimtoka ukiwaponya wote

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo.





Septemba 09, 2024
Juma la 23, Mwaka B wa kanisa

SOMO: 1Kor 5:1–8

Habari imeenea ya kuwa kwenu kuna zinaa, na zinaa ya namna isiyokuwako hata katika Mataifa, kwamba mtu awe na mke wa babaye. Nanyi mwajivuna, wala hamkusikitika, ili kwamba aondolewe miongoni mwenu huyo aliyetenda jambo hilo.
Kwa maana kweli, nisipokuwapo kwa mwili, lakini nikiwapo kwa roho, mimi mwenyewe, nimekwisha kumhukumu yeye aliyetenda jambo hilo, kana kwamba nikiwapo. Katika jina la Bwana wetu Yesu, ninyi mkiwa mmekusanyika pamoja na roho yangu, pamoja na uweza wa Bwana wetu Yesu; kumtolea Shetani mtu huyo, ili mwili uadhibiwe, ili na roho iokolewe katika siku ya Bwana Yesu. Kujisifu kwenu si kuzuri.
Hamjui kwamba chachu kidogo hulichachusha donge zima? Basi, jisafisheni, mkatoe ile chachu ya kale, mpate kuwa donge jipya, kama vile mlivyo hamkutiwa chachu. Kwa maana Pasaka wetu amekwisha kutolewa kuwa sadaka, yaani, Kristo; basin a tuifanye karamu, si kwa chachu ya kale, wala kwa chachu ya uovu na ubaya, bali kwa yasiyochachika, ndio weupe wa moyo na kweli.

Neno la Bwana...Tumshukuru Mungu


WIMBO WA KATIKATI
Zab 5:4–6, 11

Unawachukia wote watendao ubatili.
Utawaharibu wasemao uongo;
Bwana humzira mwuaji na mwenye hila.
(K) Bwana, uniongoze kwa haki yako.

Maana huwi Mungu apendezwaye na ubaya;
Mtu mwovu hatakaa kwako;
Wajivunao hawatasimama mbele za macho yako.
(K) Bwana, uniongoze kwa haki yako.

Nao wote wanaokukimbilia watafurahi;
Watapiga daima kelele za furaha.
Kwa kuwa Wewe unawahifadhi,
Walipendao jina lako watakufurahia.
(K) Bwana, uniongoze kwa haki yako.

SHANGILIO
Zab 19:8

Aleluya, aleluya,
Amri ya Bwana ni safi, huyatia macho nuru.
Aleluya

INJILI
Lk 6:6–1

Ilikuwa siku ya sabato nyingine Yesu aliingia katika sinagogi akafundisha; na mlikuwamo mtu ambaye mkono wake wa kuume umepooza. Na waandishi na Mafarisayo walikuwa wakimvizia, ili waone kwamba ataponya siku ya sabato; kusudi wapate neno la kumshitakia. Lakini yeye atakayatambua mawazo yao, akamwambia yule mwenye mkono uliopooza, Ondoka, simama katikati; akaondoka akasimama.
Ndipo Yesu akawaambia, Nawauliza ninyi, Je! Ni halali siku ya sabato kutenda mema, au kutenda mabaya; kuponya roho au kuangamiza? Akawakazia macho wote pande zote, akamwambia yule mtu, Nyosha mkono wako. Akaunyosha; mkono wake ukawa mzima tena.
Wakajawa na uchungu, wakashauriana wao kwa wao wamtendeje Yesu.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo.





Septemba 08, 2024
Juma la 23, Mwaka B wa kanisa

WIMBO WA MWANZO: Zab 119:137, 124

Ee Bwana, wewe ndiwe mwenye haki, na hukumu zako ni za adili. Kama zilivyo rehema zako umtendee mtumishi wako.


SOMO LA KWANZA: Isa 35:4-7a

Waambieni walio na moyo wa hofu, Jipeni moyo, msiogope; tazama, Mungu wenu atakuja na kisasi, na malipo ya Mungu; atakuja na kuwaokoa ninyi.
Ndipo macho ya vipofu yatafumbuliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa.
Ndipo mtu aliye kilema ataruka-ruka kama kulungu, na ulimi wake aliye bubu utaimba; maana katika nyika maji yatabubujika; na vijito jangwani. Na mchanga ung'aao mfano wa maji utakuwa ziwa la maji, na nchi yenye kiu itakuwa chemchemi za maji;

Neno la Bwana...Tumshukuru Mungu


WIMBO WA KATIKATI
Zab 146:7-10

Bwana ndiye ashikaye kweli milele,
Huwafanyia hukumu walioonewa,
Huwapa wenye njaa chakula;
Bwana hufungua waliofungwa;
(K) Ee nafsi yangu, umsifu Bwana.

Bwana huwafumbua macho waliopofuka;
Bwana huwainua walioinama;
Bwana huwapenda wenye haki;
Bwana huwahifadhi wageni;
(K) Ee nafsi yangu, umsifu Bwana.

Huwategemeza yatima na mjane;
Bali njia ya wasio haki huipotosha.
Bwana atamiliki milele, Mungu wako,
Ee Sayuni, kizazi hata kizazi.
(K) Ee nafsi yangu, umsifu Bwana.

SOMO LA PILI: Yak 2:1-5

Ndugu zangu, imani ya Bwana wetu Yesu Kristo, Bwana wa utukufu, msiwe nayo kwa kupendelea watu.
Maana akiingia katika sinagogi lenu mtu mwenye pete ya dhahabu na mavazi mazuri; kisha akiingia na maskini, mwenye mavazi mabovu; nanyi mkimstahi yule aliyevaa mavazi mazuri, na kumwambia, Keti wewe hapa mahali pazuri; na kumwambia yule maskini, Simama wewe pale, au keti miguuni pangu, je! Hamkufanya hitilafu mioyoni mwenu, mkawa waamuzi wenye mawazo mabovu?
Ndugu zangu wapenzi, sikilizeni, Je! Mungu hakuwachagua maskini wa dunia wawe matajiri wa imani na warithi wa ufalme aliowaahidia wampendao?

Neno la Bwana...Tumshukuru Mungu


SHANGILIO
Yn 8:12

Aleluya, aleluya,
Mimi ndimi nuru ya ulimwengu, asema Bwana; Yeye anifuataye atakuwa na nuru ya uzima.
Aleluya

INJILI
Mk 7:31-37

Yesu alitoka katika mipaka ya Tiro, akapita katikati ya Sidoni, akaenda mpaka bahari ya Galilaya, kati ya mipaka ya Dekapoli. Wakamletea kiziwi, naye ni mwenye utasi, wakamsihi amwekee mikono.
Akamtenga na mkutano faraghani, akatia vidole vyake masikioni mwake, akatema mate, akamgusa ulimi, akatazama juu mbinguni, akaugua, akamwambia, Efatha, maana yake, Funguka. Mara masikio yake yakafunguka, kifungo cha ulimi wake kikalegea, akasema vizuri.
Akawaonya wasimwambie mtu; lakini kadiri ya alivyozidi kuwaagiza, ndivyo walivyozidi kutangaza habari; wakashangaa mno kupita kiasi, wakinena, Ametenda mambo yote vema; viziwi awafanya wasikie, na bubu waseme.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo.





Septemba 07, 2024
Juma la 22, Mwaka B wa kanisa

SOMO: 1Kor 4:6-15

Ndugu zangu, mambo hayo nimeyafanya kuwa mfano wa mimi na Apolo kwa ajili yenu, ili kwamba kwa mfano wetu mpate kujifunza kutokupita yale yaliyoandikwa; ili mmoja wenu asijivune kwa ajili ya huyu, kinyume cha mwenziwe. Maana ni nani anayekupambanua na mwingine? Nawe una nini usichokipokea?

Lakini iwapo ulipokea, wajisifia nini kana kwamba hukupokea? Mmekwisha kushiba, mmekwisha kupata utajiri, mmemiliki pasipo sisi. Naam, laiti mngemiliki, ili sisi nasi tumiliki pamoja nanyi! Maana nadhani ya kuwa Mungu ametutoa sisi mitume mwisho, kama watu waliohukumiwa wauawe; kwa sababu tumekuwa tamasha kwa dunia; kwa malaika na wanadamu. Sisi tu wapumbavu kwa ajili ya Kristo, lakini ninyi ni wenye akili katika Kristo; sisi tu dhaifu, lakini ninyi mna nguvu; ninyi mna utukufu, lakini sisi hatupati heshima.

Hata saa hii ya sasa, tuna njaa na kiu, tu uchi, twapigwa ngumi, tena hatuna makao; kisha twataabika tukifanya kazi kwa mikono yetu wenyewe. Tukitukanwa twabariki, tukiudhiwa twastahimili; tukisingiziwa twasihi; tumefanywa kama takataka za dunia, na tama ya vitu vyote hata sasa. Siyaandiki hayo ili kuwatahayarisha; bali kuwaonya kama watoto niwapendao. Kwa kuwa ijapokuwa mna waalimu kumi elfu katika Kristo, walakini hamna baba wengi. Maana mimi ndimi niliyewazaa katika Kristo Yesu kwa njia ya Injili.

Neno la Bwana...Tumshukuru Mungu


WIMBO WA KATIKATI
Zab 145:17-21

Bwana ni mwenye haki katika njia zake zote,
Na mwenye fadhili juu ya kazi zake zote.
Bwana yu karibu na wote wamwitao,
Wote wamwitao kwa uaminifu.
(K) Bwana yu karibu na wote wamwitao.

Atawafanyia wamchao matakwa yao,
Naye atakisikia kilio chao na kuwaokoa.
Bwana huwahifadhi wote wampendao,
Na wote wasio haki atawaangamiza.
(K) Bwana yu karibu na wote wamwitao.

Kinywa changu kitazinena sifa za Bwana;
Wote wenye mwili na walihimidi jina lake takatifu milele na milele.
(K) Bwana yu karibu na wote wamwitao.

SHANGILIO
Yn 14:6

Aleluya, aleluya,
Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi.
Aleluya

INJILI
Lk 6:1-5

Ilikuwa siku ya sabato moja alikuwa akipita katika mashamba, wanafunzi wake wakawa wakivunja masuke na kuyala, wakiyapukusa-pukusa mikononi mwao.
Basi baadhi ya Mafarisayo wakawaambia, Mbona mnafanya lisilo halali siku ya sabato? Yesu akawajibu akawaambia, Hamkulisoma hata hilo alilolifanya Daudi, alipokuwa na njaa, yeye na wale aliokuwa nao? Jinsi alivyoingia katika nyumba ya Mungu, akaitwaa mikate ile ya Wonyesho, akaila akawapa na hao wenziwe, ambayo si halali kuila ila kwa makuhani peke yao.
Akawaambia, Mwana wa Adamu ndiye Bwana wa sabato.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo.





Septemba 6, 2024
Juma la 22, Mwaka B wa kanisa

SOMO: 1Kor 4:1–5

Mtu na atuhesabu hivi, kuwa tu watumishi wa Kristo, na mawakili wa siri za Mungu. Hapo tena inayohitajiwa katika mawakili, ndiyo mtu aonekane kuwa mwaminifu.

Lakini, kwangu mimi, si kitu kabisa nihukumiwe na ninyi, wala kwa hukumu ya kibinadamu, wala sijihukumu hata nafsi yangu. Maana sijui sababu ya kujishitaki nafsi yangu, lakini sihesabiwi haki kwa ajili hiyo; ila anihukumuye mimi ni Bwana.

Basi ninyi msihukumu neno kabla ya wakati wake, hata ajapo Bwana; ambaye atayamulikisha yaliyositirika ya giza, na kuyadhihirisha mashauri ya mioyo; ndipo kila mtu atakapoipata sifa yake kwa Mungu

Neno la Bwana...Tumshukuru Mungu


WIMBO WA KATIKATI
Zab 37:3–6, 27, 28, 39–40

Umkabishi Bwana njia yako,
Pia umtumaini, naye atafanya.
Atajitokeza haki yako kama nuru,
Na hukumu yako kama adhuhuri.
(K) Wokovu wa wenye haki una Bwana.

Umtumaini Bwan aukatende mema,
Ukae katika nchi, upendezwe na uaminifu.
Nawe utajifurahisha kwa Bwana,
Naye atakupa haja za moyo wako.
(K) Wokovu wa wenye haki una Bwana.

Jiepue na uovu, utende mema,
Na kukaa hata milele.
Kwa kuwa Bwana hupenda haki,
Wala hawaachi watauwa wake.
(K) Wokovu wa wenye haki una Bwana.

Na wokovu wa wenye haki una Bwana;
Yeye ni ngome yao wakati wa taabu.
Naye Bwana huwasaidia na kuwaopoa;
Huwaopoa na wasio haki na kuwaokoa;
Kwa kuwa wamemtumaini Yeye.
(K) Wokovu wa wenye haki una Bwana.

SHANGILIO
Zab 25:4,5

Aleluya, aleluya,
Ee Bwana, unijulishe njia zako, unifundishe mapito yako.
Aleluya

INJILI
Lk 5:33–39

Mafarisayo na waandishi walimwambia Yesu, Wanafunzi wa Yohane hufunga mara nyingi, na kuomba dua; na kadhalika wanafunzi wa Mafarisayo; lakini wanafunzi wako hula na kunywa!

Lakini Yesu akawaambia, Je! Mwaweza kuwafanya wafunge walioalikwa arusini, akiwapo bwana arusi pamoja nao? Lakini siku zitakuja watakapoondolewa bwana arusi, ndipo watakapofunga siku zile.

Akawaambia na mithali, Hakuna akataye kiraka cha vazi jipya na kukitia katika vazi kuukuu; na kama akitia, amelikata lile jipya, na kile kiraka cha vazi jipya hakilingani na lile vazi kuukuu. Wala hakuna mtu atiaye divai mpya katika viriba vikuukuu; na kama akitia, ile divai mpya itavipasua vile viriba, divai yenyewe itamwgika, na viriba vitaharibika.

Lakini divai mpya sharti kutiwa katika viriba vipya. Wala hakuna anyway divai ya kale akatamani divai mpya; kwa kuwa asema, Ile ya kale ndiyo iliyo njema.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo.


Kwa masomo ya misa za kila siku, Sala mbalimbali na historia za maisha ya watakatifu tembelea catholickigomadiocese.org